Na Mashaka Mgeta, SAADANI
UMBALI wa takribani kilomita 131 kutoka jijini Tanga, inapatikana Hifadhi ya Taifa ya Saadani, mahali palipofanyika kikao cha Baraza la Wafanyakazi mkoani Tanga Januari 27 na 28, 2026.
Wajumbe wa kikao hicho kutoka wilaya nane za Mkoa wa Tanga, wamekutana kwenye hifadhi hiyo yenye upekee wa kuwa ufukweni wa Bahari ya Hindi.
Katibu Tawala Mkoa wa Tanga, Rashid Mchatta, anafungua kikao hicho kwa kuwahimiza watumishi wa umma kuwekeza zaidi kwenye utendaji kazi wenye tija na ufanisi kupitia utoaji huduma kwa jamii.
Mchatta anasema Serikali ya Mhe Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, inatimiza wajibu msingi wa kuwalipa watumishi stahiki zao inavyostahili na kwa wakati, hivyo ni jukumu lao (watumishi) kuitafsiri hali hiyo kama deni linalopaswa kulipwa kupitia utendaji kazi wao.
“Mazingira yaliyopo kwa watumishi wa umma ni wezeshi, yanayotoa hakika ya kufanya kazi ili kufikia malengo ya kuwatumikia wananchi…hili deni tunalipaswa kulilipa kwa kufanya kazi kwa ufanisi ili tija ipatikane,” akasema.
Pia, Mchatta amewaasa watumishi katika Sekretarieti ya Mkoa huo, kuzisaidia Mamlaka za Serikali za Mitaa kubuni fursa mpya za uwekezaji na miradi itakayochangia kuinua pato la taifa, kuboresha na kustawisha maisha ya watu.
Naye Katibu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya (TUGHE) wa Mkoa wa Tanga, Straton Lufyagila, ameiongoza Sekretarieti ya Mkoa wa Tanga kwa kufanikisha kikao hicho, na kufanikisha kuwa cha wazi, haki na usawa katika kujadili masuala yanayowahusu watumishi.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.