Kikao cha Mkoa cha Tathimini ya utekelezaji wa shughuli za Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) kwa robo mwaka ya kuanzia mwezi Oktoba mpaka Disemba, kimefanyika Wilayani Pangani tarehe 22/02/2018.
Kikao hicho kilichoandaliwa na kufanyika kwa ufadhili wa shirika la GIZ Mkoa wa Tanga kimehudhuriwa na washiriki mbalimbali wakiwemo wahe. Wakuu wa Wilaya, wahe. Wenyeviti wa Halmashauri, Wakurugenzi wa Jiji, Miji na Halmashauri, Waganga wakuu wa Halmashauri, Maafisa Mipango na Waratibu wa CHF. Pia kikao hicho kilihudhuriwa na wawakilishi wa mashirika mbalimbali yanayotoa huduma za Afya kwa jamii kwa kushirikiana na Serikali (PPP) likiwemo shirika la CSSC. Wawakilishi wa MSD, NHIF na Wizara ya Afya pia walikuwepo.
Baada ya kuona tathimini ya hali ya Utekelezaji wa shughuli za CHF na maoni mbalimbali kutoka kwa washiriki, mgeni Rasmi na Mwenyekiti wa kikao hicho Mkuu wa Mkoa wa Tanga mhe. Martin Shigella aliwapongeza washiriki wote kwa kazi nzuri waliyoifanya na kuwataka waongeze nguvu katika kuhamasisha wananchi kujiunga na mfuko wa CHF kwani ni rahisi kwa mwananchi aliyejiunga na Mfuko wa CHF kupata huduma za Afya kuliko yule ambaye hajajiunga. Pia aliwaomba kutafuta namna nzuri ya kuwaangalia wazee na walemavu kwa kuwakatia kadi za CHF ili nao wapate huduma za Afya kwa urahisi bila usumbufu wowote. Mhe. Mkuu wa Mkoa amewaagiza Wakurugenzi kuhakikisha wanaidhinisha na kusimamia pesa za miradi kwa wakati ili kuepuka fedha hizo kubaki wakati wananchi wanahitaji huduma bora.
Awali ya hapo waratibu wa CHF kutoka kila Halmashauri walitoa taarifa fupi kuhusu mwenendo na utekelezaji wa shughuli za CHF katika maeneo yao. Mratibu wa CHF Mkoa alihitimisha kwa kuonyesha hali halisi ya Utekelezaji wa CHF hadi Disemba 2017, ambapo alionyesha kuwa:-
(i) Robo ya Julai - Septemba 2017 kulikuwa na jumla ya kaya 259,751 (63%) zilizojiunga na mfuko wa afya ya Jamii (CHF).
(ii) Robo ya Oktoba - Disemba 2017 jumla ya kaya 290,377 (70%) zimejiunga na mfuko wa Afya Jamii (CHF).
(iii) Jumla ya kaya 30,626 (7.4%) zimeongezeka kupitia Halmashauri zetu.
(iv) Ongezeko kubwa katika robo hii (Oktoba - Disemba 2017) limetokana na malipo ya KWF yaliyolipwa kwa ajili ya wategemezi wa akina mama 47,294 ambazo ni Jumla ya Tshs. 526,240,000.
Pamoja na ufadhili wa vikao vya kila robo mwaka, GIZ wamekuwa wakiziwezesha Halmashauri za Mkoa wa Tanga vitendea kazi kama vile Kompyuta, Printer, friji na Stoo za dawa.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.