Na Mashaka Mgeta, KILINDI
UKUBWA wa uhitaji wa barabara ya lami inayoiunganisha Wilaya ya Kilindi na makao makuu ya Mkoa wa Tanga, unaonekana kupitia magoti yaliyopigwa na wabunge wawili kwa Waziri Mkuu, Mhe Dkt Mwigulu Nchemba.
Mbunge wa Kilindi, Mhe Mbwana Mhando (Pichani akizungumza na Mhe Mwigulu) na Mhe Jumaa Aweso wa Pangani, ambaye pia ni Waziri wa Maji, wamefanya hivyo kwa nyakati tofauti wakati wa ziara ya Mhe Dkt Mwigulu wilayani Kilindi jana Februari 14, 2026.
Mhe Dkt Mwigulu alikuwa kwenye hafla ya uwekaji jiwe la msingi kwenye Hospitali ya Wilaya, alipotoa fursa kwa viongozi kadhaa kuzungumza, wakiwemo Wahe. Aweso na Mhando.
Alianza Mhe Mhando, ambaye baada ya kuelezea maendeleo makubwa yaliyofikiwa kwenye sekta mbakimbali wilayani humo, akasema barabara ya lami hiyo inaendelea kuwa hitaji ambalo halijafanyiwa kazi kwa kiwango cha kuridhisha.
Barabara ya Handeni – Songe Kilindi ni sehemu ya mradi wa barabara ya Handeni - Kibirashi - Kiteto - Kwamtoro Singida yenye urefu wa kilomita 340.
Kati ya urefu huo kuna kilomita 50 za kutoka Handeni – Mafleta – Kireguru zimepata wakandarasi, na nyingine yenye urefu wa kilomita 63 kufika eneo yalipo makao makuu ya Wilaya ya Kilindi zinatarajiwa kutangazwa hivi karibuni.
Akiwa amepiga magoti, pengine kuonesha heshima na ushuhuda wa kudhamiria, Mhe Mhando akasema ujenzi wa barabara ya Handeni - Kilindi yenye urefu wa km 113 ulianza kuwekwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) tangu mwaka 2005, hivyo ipo haja ya kuongeza bidii ili mpango utakaofanikisha kukamilika kwake ufanikiwe.
Kwa mujibu wa Mhe Mhando, barabara hiyo itakapokamilika kwa kiwango cha lami, itachochea maendeleo ya watu, miundombinu, uwekezaji na huduma za kijamii zenye kukuza uchumi na ustawi wa wqkazi wake.
Naye Mh Aweso, akinukuu neno la ki-imani linalosema, “unapowazulu wengine usinipite Bwana’, Mhe. Aweso akipiga goti moja kwa ishara ile ya Mhe Mhando, akasema kuna kila sababu ya kuamini kwamba Kilindi wana uhitaji na wanastahili kujengwa barabara hiyo ya lami.
Naye Naibu Waziri wa Ujenzi, Mhe Godfrey Kasekenya alisema barabara ya Handeni- Kibirashi - Kiteto - Singida ilitolewa maelekezo na Mh Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, ijengwe kwa Ushirikiano wa Sekta ya Umma na Binafsi (PPP).
Amesema, wizara hiyo imewasiliana na Mamlaka ya Bandari (TPA) na Wakala wa Barabara (TANROADS) na kufanya mapitio mapya ya ujenzi wa barabara hiyo na kwamba hatua za utelekezaji zipo katika hatua za mwisho, huku ikichukuliwa tahadhali kwa vile ni mara ya kwanza ujenzi wa barabara kufanyika kwa njia hiyo.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.