Na Mashaka Mgeta, MKINGA
CHUO Kikuu cha Mzumbe kimetangaza kuwekeza zaidi kwenye programu za kukuza ujuzi kwa vijana wanataaluma, ili kukidhi uendelezaji rasilimali zilizopo kwenye maeneo mbalimbali nchini.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Profesa Daniel Mushi ameyasema hayo alipozungumza kwenye hafla ya kuweka jiwe la msingi kwenye ujenzi wa Kampasi ya Tanga ya Chuo hicho iliyopo wilayani Mkinga.
Hafla ya uwekaji jiwe la msingi imehudhuriwa na viongozi wa ngazi mbalimbali serikalini na taasisi binafsi, na wananchi ambapo mgeni rasmi alikuwa Waziri Mkuu, Mhe Dkt Mwigulu Nchemba.
Profesa Mushi ametoa mfano kuwa azma hiyo itatekelezwa kwenye Kampasi ya Mkinga ambayo miongoni mwa maeneo ya ujuzi yatakayotiliwa mkazo katika ufundishaji ni kuhusu matumizi na uendelezaji wa rasilimali za baharini.
Mradi wa Kampasi ya Tanga ya Chuo Kikuu cha Mzumbe unaogharimu Shilingi 16,015,580,000 unajengwa kwa ushirikiano wa Serikali na Benki ya Dunia (WB).
Profesa Mushi amesema chuo hicho kinachotarajiwa kudahili wanafunzi kwa kipindi cha masomo kianzia Oktoba mwaka huu, kitawalenga wanafunzi waliomaliza kidato cha sita na waliomaliza kidato cha nne watakaoanzia ngazi ya stashahada.
Amesema, Mzumbe inatambua ongezeko la vijana wanaohitimu vidato vya nne na sita, hasa baada ya mafanikio makubwa ya utoaji elimu ya msingi bila malipo.
Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe Balozi Dkt Batilda Burian, amesema ujenzi wa Kampasi hiyo ni mwendelezo uboreshaji sekta elimu ambapo kwa mwaka 2025/2026, mkoa huo ulipokea Shilingi bilioni 359.
Anasema fedha hizo zilitolewa kwa ujenzi wa miundombinu kama shule mpya za msingi na sekondari, Vyuo vya Ufundi Stadi (VETA), miongoni mwa mingine.
Mwenyekiti wa Baraza la Wadhamini wa Mzumbe, Profesa Saida Yahya-aothman amesema uwepo wa Kampasi hiyo wikayani Mkinga, unatokana na uhakika wa mazingira bora kwa kufundisha, kujifunza na kushiriki elimu ya vitendo, kwa kuzingatia mahitaji ya soko la ajira.
Hata hivyo, Profesa Saida amesema chuo hicho kinahitaji kufikishiwa huduma muhimu kama vile maji, umeme ili kusiwepo kikwazo wakati wa kuanza mwaka wa masomo utakapoanza.
Waziri Mkuu, Mhe Dkt Mwigulu, amezielekeza Wizara ya Nishati, Wizara ya Maji na Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kuhakikisha huduma hizo zinafikishwa chuoni hapo kabla ya Oktoba, mwaka huu.
Amesema, uwekezaji wa Chuo hicho ni miongoni mwa miradi inayoiheshimisha nchi, na kuwa ishara halisi ya dhamira ya Mhe Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kuwatumikia wananchi.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.