Na Mashaka Mgeta, OMM TANGA
DHANA ya 'fekeo na rato' vinavyoashiria utayari wa Waziri Mkuu, Mhe Dkt. Mwigulu Nchemba kuchochea utendaji kazi bora serikalini, uwajibikaji na udhibiti ubadhirifu wa mali ya umma, inaonekana kwa vitendo.
Akiwa katika ziara yake mkoani Tanga kuanzia Februari 13, 2026, Mhe Dkt. Mwigulu, anasema pamoja na kutembelea, kukagua, kuweka mawe ya msingi ama kufungua miradi ya maendeleo, pia anashughulikia 'mambo yanayokwama' kwenye miradi ya maendeleo, huduma za ustawi na sababu za mkwamo husika.
Anasema, sehemu ya mikwamo hiyo inatokana na sababu zinazotumika kama 'vichaka vya ubadhirifu wa mali ya umma', vinavyofanywa na watumishi wa umma wasiokuwa waadilifu, wanaoichafua Serikali ya Mhe Rais Dkt Samia Suluhu Hassan.
Mathalani, akiwa wilayani Handeni, Mhe Dkt Mwigulu alibaini kuwepo milango 34 isiyokuwa na ubora, iliyowekwa kwenye Kituo cha Afya na kuganda kwa mifuko 1,262 ya saruji iliyotakiwa kutumika kwenye ujenzi wa Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) wilayani Handeni.
Pia, Mhe Dkt Mwigulu amebaini kuwepo mkandarasi Hamimu Kusaga wa kampuni ya Green Construction iliyoshinda zabuni ya mradi wa ukarabati na upanuzi katika Mji Mdogo Mombo wilayani Korogwe, kuondoka na fedha alizolipwa huku akiutekeleza mradi huo wenye thamani ya Shilingi xxxx
Mhe Dkt Mwigulu ameiagiza Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kufanya uchunguzi wa kina na haraka kwenye maeneo hayo, na kumpatia taarifa ikihusisha majina ya wahusika, kwa hatua zaidi.
Amesema, kwa mradi wa VETA ulio chini ya usimamizi wa Wizara ya Elimu, Katibu Mkuu wa wizara hiyo awachukulie hatua wahusika, ikiwa ni pamoja na kuwakata mishahara yao ili fedha hizo zitumike kununua saruji iliyoganda.
"Nikiyafanya haya watu wanasema nimekuwa mkali na kwamba nitachukiwa, sijaja hapa kupendwa, nipo hapa kusafisha vichaka vya ubadhirifu na wizi wa mali za umma," anasema.
Mhe Dkt Mwigulu anasema, kuna ishara za wazi kuwepo mbinu kwa watumishi wasiokuwa waaminifu, kutumia mifumo yenye kuhalalisha ukubwa wa gharama hasa kwenye ujenzi wa miundombinu mbalimbali, ili kujinufaisha.
Anaonya, "fedha za umma ni za kuogopa, usidhani ni kama matunda pori kila anayepita anachuma...ninawaonya watumishi na wadau wetu katika sekta binafsi, msihiriki ubadhirifu ama wizi wa mali ya umma," anasema.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.