Katika kuhakikisha Wananchi wa Mkoa wa Tanga wanapata huduma bora na kutatuliwa kero zinazowasumbua kwa muda mrefu, Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Martin Shigela ametembelea wananchi wa Wilaya ya Mkinga tarehe 10/07/2017 ili kujua changamoto mbalimbali zinazowakabili na kuzitafutia ufumbuzi wa haraka na wenye tija. Katika ziara hiyo Mhe. Mkuu wa Mkoa alianza kwa kukutana na kamati ya ulinzi na usalama ngazi ya wilaya. Kamati ya ulinzi na usalama chini ya Mkuu wa Wilaya ya Mkinga Mhe. Yona Maki ilimhakikishia Mkuu wa Mkoa kuwa hali ya usalama katika Wilaya ya Mkinga ni shwari, chakula kipo cha kutosha na wananchi wamezuiliwa kusafirisha chakula nje ya nchi mpaka kwa kibali maalum kama alivyoagiza Mhe. Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pia kamati ilimhakikishia Mhe. Mkuu wa Mkoa kuwa Mipaka ya nchi imedhibitiwa vizuri na hakuna tishio lolote kwa sasa, wahamiaji haramu nao wamedhibitiwa. Baada ya hapo Mhe. Mkuu wa Mkoa alihudhuria Mkutano maalum wa Baraza la Madiwani kwa ajili ya kupitia majibu ya hoja za ukaguzi wa hesabu za Halmashauri kuishia Juni 30. 2016. Mhe. Mkuu wa Mkoa aliwahimiza wahe. Madiwani na Mkurugenzi Mtendani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga kuhakikisha wanatenga fedha kwa ajili ya kuchangia mfuko wa akina mama na vijana. Pia Mhe. Mkuu wa Mkoa aliagiza Mwanasheria aliyeisababishia hasara Halmashauri kwa kushindwa kuhudhuria kwenye kesi Mahakamani akamatwe popote alipo na afikishwe kwenye vyombo vya sheria. Mhe. Mkuu wa Mkoa aliwapa habari njema wahe. Madiwani kuwa Mhe. Rais anatarajia kuja Mkoani Tanga hivi karibuni kwa ajili ya kuweka jiwe la msingi kwenye Bomba la mafuta na kiwanda kikubwa cha Saruji. Mhe. Mkuu wa Mkoa aliwasisitiza watendaji wa Halmashauri pamoja na Wahe. Madiwani kuhusu matumizi mazuri ya fedha, wajiepushe na tamaa, na wahakikishe kila shilingi ya Serikali inayotumika thamani yake ionekane kwa kutoa huduma bora kwa wananchi. Baada ya hapo Mhe. Mkuu wa Mkoa alienda kukagua ujenzi wa shule ya Sekondari Mkinga Leo katika Kata ya Mkinga. Ujenzi wa Madarasa manne (4) na ofisi moja ya walimu umekamilika pamoja na vyoo vyake. Hivyo Mhe. Mkuu wa Mkoa aliruhusu Shule hiyo ifunguliwe na wiki ijayo wanafunzi wa Kidato cha Tano waanze masomo. Kidato cha kwanza mpaka cha nne ni mchanganyiko, na kidato cha tano na cha sita ni Wasichana tu. Baada ya kuikagua shule ya sekondari Mkinga Leo Wasichana Mhe. Mkuu wa Mkoa alikutana na Wananchi wa Kata ya Mkinga katika Mkutano wa hadhara, ambapo wananchi waliuliza maswali na kutoa kero mbalimbali ambazo zilijibiwa na Mhe. Mkuu wa Mkoa akisaidiana na Mbunge wa jimbo la mkinga, Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga na watendaji wengine wa Serikali waliohudhuria Mkutano huo.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.