Na Mashaka Mgeta, HANDENI
AHADI ya Mbunge wa Handeni Mjini, Mhe Reuben Kwagilwa, kuoga hadharani pindi maji yanayotokana na uboreshwaji wa miundombinu ya mradi wa maji wa Handeni Truck Main (HTM) yatakapotoka, inamuibua Waziri wa Maji, Mhe Jumaa Aweso.
Mhe Kwagilwa ambaye pia ni Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali (TAMISEMI), mbele ya Waziri Mkuu, Mhe Dkt Mwigulu Nchemba, akairejea ahadi ya kuoga hadharani akiwa amevaa nguo, kuashiria furaha ya kupatikana maji yaliyo miongoni mwa kero zilizodumu muda mrefu wilayani Handeni.
Kauli ya Mhe Kwagilwa inakuwa sababu kwa Mhe Aweso, kutoa ufafanuzi wa hoja hiyo na nyingine zilizoibuliwa na wananchi kwenye mkutano wa hadhara uliohutubiwa na Mhe Mwigulu kwenye uwanja wa Handeni Square.
Mhe Aweso, anathibitisha kuwepo kero ya maji Handeni na kusema zipo hatua mbalimbali zinaendelea kuchukuliwa na Serikali ya Mhe Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, kuondokana na kadhia hiyo.
Kwa mujibu wa Mhe Aweso, hatua hizo ni pamoja na utekelezaji wa mradi wa HTM unaolenga kubadilisha miundombinu kutoka iliyokuwa tangu mwaka 1974 na kuweka ya kisasa, kupitia mradi unaogharimu Shilingi bilioni 171.
Mhe Aweso, kama vile ‘amejitwisha mzigo’ wa dhamana kwa wakazi wa Handeni, anasema mradi huo utakamilika muda mfupi ujao, na baada ya Bunge litakalofanya mkutano na vikao vyake kuanzia mwishoni mwa Machi mwaka huu, mradi huo utazinduliwa na hivyo kuyafanya maji ‘yatiririke’ wilayani Handeni kwa muda wote.
Ahadi hiyo inaibua shangwe na nderemo kwa wakazi wa mji huo, wakirejea kauli ya awali ya Mhe Aweso kwamba, wakati maeneo mengine yana shida ya maji, Handeni kuna dhiki ya maji.
Mhe Aweso amesema pamoja na hatua hiyo, zipo juhudi za Serikali kujenga mabwawa kwenye maeneo ya Kibaya, Nkale, Kweingoma, Kwa Msangazi na Msasa, ili kuondokana na kadhia hiyo.Waziri wa Kilimo, Mhe Daniel Chongolo, akasema uhakika wa maji kwa jamii, ni sehemu muhimu inayovutia uwekezaji na viwanda, huku ikichagiza upatikanaji chakula cha mifugo kwenye nyanda za malisho.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.