Na Mashaka Mgeta, HANDENI
WAZIRI Mkuu, Mhe Dkt. Mwigulu Nchembe, ameionya jamii kuepuka vitendo na kauli zinazotengeneza na kukuza ufa wa uadui kupitia migororo ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji.
Mhe Dkt. Mwigulu, ameyasema hayo leo Februari 13, 2026, alipozugumza baada ya kusikiliza kero za wananchi katika hafla ya uwekaji jiwe la msingi kwenye Kituo cha Kupooza Umeme kilichopo Mkata wilayani Handeni Mkoa wa Tanga.
Alikuwa akijibu swali na mkazi wa Kijiji cha Mkata Mashariki, Omar Athuman, aliyetaka kujua mpango wa Serikali kudhibiti migogoro kati ya jamii hizo zinazoathiri mali na maisha ya watu.
Mhe Dkt. Mwingulu amesema, kwa nyakati tofauti, kuna makosa yanayomhusisha mtu mmoja, mathalani mfugaji, lakini yanakuzwa na kuwajumuisha wafugaji wote isivyo sawa.
Amesema, kama kuna mfugaji ama mkulima anatenda kosa, inastahili tafsiri ya kadhia hiyo ‘imlenge’ mhusika na hatua kuchukuliwa dhidi yake badala ya kuelekezwa kwa jamii nzima.
Pia, Mhe Dkt Mwigulu ameasa wananchi kufuata Sheria, Kanuni na Taratibu zinazojenga msingi wa uhuru wa kila raia kuishi mahali popote, ili kuepuka migogoro kama inayotokea kati ya wakulima na wafugaji.
“Tunaruhusiwa kuishi mahali popote lakini lazima tufuate Sheria, Kanuni na Taratibu ili kuepuka jeuri na kiburi vinavyosababisha uchokozi kama wa wafugaji kulisha mifugo kwenye mazao ya wakulima,” amesema.
Mh. Dkt Mwigulu, amemuagiza Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe Balozi Dkt Batilda Burian na Kamati ya Usalama (KU) ya Mkoa huo, ‘kutowafumbia macho’ watu wanaovunja sheria, kwa vile, kutofanya hivyo kutahatarisha amani kwa watu na taifa.
Waziri wa Kilimo, Mhe Daniel Chongolo, amesema Serikali inatekeleza mipango yenye lengo la kuboresha na kuweka suluhu ya kudumu katika kudhibiti migogoro ya wafugaji na wakulima.
Amesema, miongoni mwa yanayotekelezwa kwenye mipango hiyo ni matumizi bora ya ardhi ambapo pamoja na mambo mengine, unatenganisha maeneo ya kilimo na ufugaji.
Nyingine ni matumizi ya daftari la makazi maeneo ya vijiji, litakalowezesha kuwatambua wakazi halali, hivyo kuwadhibiti wavamizi kwenye maeneo wasiyotakiwa.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.