Na Emma Kigombe, KOROGWE
KATIBU Tawala Mkoa (RAS) wa Tanga, Pili Mnyema leo Tarehe 12, Julai 2024, ameongoza kikao kazi cha Maafisa Tarafa wa mkoani humo kilichofanyika wilayani Korogwe.
Akizungumza kwenye kikao hicho cha siku moja, RAS Mnyema amewataka Maafisa Tarafa hao kuhakikisha wanafanya kazi kwa bidii na maarifa katika kuwatumikia wananchi ipasavyo.
Amesema, Mhe Rais Dk Samia Suluhu Hassan ameweka mazingira mazuri zaidi yaliyowapa fursa pana Maafisa Tarafa hao wanaojulikana pia kama Magavana kwenye maeneo yao, kutekeleza majukumu yao ipasavyo na kwa ufanisi.
RAS Mnyema ametoa mfano wa mazingira bora yaliyopo kwa Maafisa Tarafa hao kuwa ni uwepo wa ofisi za kisasa na makazi bora ya kuishi, ambapo takwimu zinaonyesha kuwa huduma hizo zipo kwenye tarafa zote 37 mkoani humu.
“Tuna kila sababu ya kumshukuru Mhe. Rais Dk Samia, lazima tumlipe kwa kufanya kazi kubwa ya kuwatumikia watanzania katika mkoa wetu,” amesema RAS Mnyema.
Aidha, RAS Mnyema amewasisitiza viongozi hao kuenenda katika maadili ya utumishi wa umma, ili kujenga uhusiano mzuri na wananchi na kushirikiana nao katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo kwa maslahi mapana ya mkoa wa Tanga na Taifa kwa ujumla.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.