Na Mashaka Mgeta, KOROGWE
WAZIRI Mkuu, Mhe Dkt. Mwigulu Nchemba, ameagiza kusakwa na kuwekwa ndani Mkurugenzi wa kampuni ya Greens Construction Limited, Hamimu Kusaga, anayedaiwa kulipwa Shilingi milioni 934 za mradi wa ukarabati na upanuzi wa katika mji mdogo wa Mombo, kisha kuutelekeza.
Mhe Dkt Mwigulu amesema, mkandarasi huyo anayedaiwa kuishi jijini Dodoma atakapopatikana, anapaswa kusakwa, kukamatwa na kuwekwa ndani hadi atakaporejesha fedha hizo, kisha hatua nyingine za kisheria kuchukuliwa.
Ili kufanikisha azma hiyo, Mhe Dkt. Mwigulu, amemuagiza Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe Balozi Dkt. Batilda Burian, kuwasiliana na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe Rosemary Senyamule, ili mkandarasi huyo akamatwe na kufikishwa Korogwe kurejesha fedha alizolipwa.
“Fedha za umma si kama matunda ya porini ambayo kila mtu anapita na kuchuma na kuondoka zake...haya ndio mambo yasiyovumilika,” amesema.
Awali, Mkuu wa Wilaya ya Korogwe, Mhe William Mwakilima, alisema mtuhumiwa huyo alilipwa fedha hizo kwa kipindi cha takribani miaka miwili iliyopita, na mchakato wa kumfungulia mashtaka unaendelea.
Akizungumzia mradi wa maji miji 28, Mhe Dkt. Mwigulu amesema ni matokeo ya nia na dhamira ya Mhe Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, kuwatumikia Watanzania kupitia utoaji huduma kwa maendeleo na ustawi wa watu.
Mhe Dkt Mwigulu alielekeza, kutokana na matokeo ya dhamira hiyo inayoonekana pia kwenye miradi mingine nchini, watu wasimame kama ishara ya kumheshimisha Mhe Rais Dkt. Samia, ikawa hivyo.
Naye Waziri wa Maji, Mhe Jumaa Aweso, alisema mradi huo unaosimamiwa na Handeni Truck Main (HTM), utagharimu Shilingi bilioni 171 na kuwanufaisha wakazi wa wilaya za Korogwe, Muheza na Pangani.
Amesema, awali, mradi huo wenye miundombinu iliyojengwa mwaka 1974 na kuwa chakavu, ulikuwa na uwezo wa kutoa lita za ujazo milioni 4 kwa watu 180,000 ,lakini utakapokamilika utatoa lita za ujazo milioni 52 kwa siku, ukiwanufaisha watu 860,000.
Wananchi wa wilaya hizo, wamepongeza jitihada za Serikali kufanikisha mradi huo utakawaondoa kwenye kadhia ya ukosefu wa maji ya uhakika iliyokuwepo kwa miongo kadhaa sasa.
Akizunguma kwa niaba ya wenzake, Hamza Matebe, mkazi wa Gitu “tunaona kwa vitendo namna Serikali ya Mhe Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, inavyotuletea maji, hii inakwenda kujenga historia isiyofutika kwa wilaya za Korogwe, Muheza, Handeni na Pangani.”
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.