SERIKALI Mkoani Tanga imesema maandalizi ya awali ikiwemo utafiti wa udongo katika maeneo yatakayowekwa miundombinu ya Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki kutoka Uganda hadi Chongoleani mkoani Tanga, yanaendelea vizuri.
Akizungumza na Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, waliomtembelea ofisini kwake Mkuu wa Mkoa wa Tanga Omary Mgumba amesema tayari maeneo kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya kambi mkoani hapa inaendelea vizuri ikiwemo fidia kwa wananchi kupisha ujenzi wa bomba imeshatolewa.
“Mradi unaendelea kwa kasi naamini utakamilika kwa wakati kama yalivyo matarajio ya serikali na wananchi,” amesema Mgumba.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, Daniel Sillo ameishauri serikali kuhakikisha inasimamia kwa ukaribu utekelezaji wa mradi ili ukamilike kwa wakati na kuleta tija ya kiuchumi kwa wananchi na taifa kwa ujumla.
“Kamati tumeridhishwa na jitihada kubwa ambazo serikali imechukua ikiwemo maandalizi mbalimbali ya ujenzi wa mradi huo ambao ukikamilika utafungua fursa za kiuchumi za nchi yetu,” amesema Sillo.
Naye Msimamizi wa mradi huo Safiel Msofe, amesema mradi huo umezingatia taratibu za kimataifa za fidia hivyo watahakikisha wananchi wanapata stahiki zao za fidia kwa mujibu wa taratibu zilizopo.
“Wananchi 388 tayari hadi sasa wameshalipwa fidia ya TShs Bilioni 2.4, kupisha maeneo yao yatayopitiwa na miundombinu ya ujenzi huo.
“Kwa sasa wananchi 6,134 ambao wapo kwenye eneo la mkuzi taratibu zinaendelea za kuhakikisha nao wanalipwa fidia zao kupisha maeneo yao tayari kwa utekelezaji wa mradi huo,” alisisitza zaidi.
Mwisho.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.