Na Mashaka Mgeta, OMM TANGA
NI mfululizo wa masimulizi ya mafanikio, pale mhimili unaotafsiri sheria na kutenda haki, yaani Mahakama, unajiweka wazi namna matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) yanavyofuta rushwa na ukiritimba kwenye utendaji kazi wake.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Tanga, Katarina Mteule (anayekagua gwaride), ameyasema hayo leo Februari 2, 2026, alipohutubia kwenye Maadhimisho ya Siku ya Sheria mkoani humo.
Jaji Mfawidhi Katarina anasema matumizi ya TEHAMA mahakamani, yanayoendelea kuboreshwa, yanayoondoa u-lazima wa mteja kuonana ‘uso kwa uso’ na mtoa huduma, hali inayodhibiti vitendo viovu vya baadhi ya watumishi hasa katika rushwa na ukiritimba.
“Maboresho hayo yamewezesha kubadilishana taarifa kwa urahisi, kupunguza ucheleweshaji wa mashauri, kurahisisha taratibu za kisheria na kuondoa tuhuma za rushwa kwani mteja anatumia mfumo zaidi,” amesema.
Ametoa mfano kuwa, kutokana na matumizi ya TEHAMA, muda wa juu wa kusikiliza shauri mkoani Tanga katika Mahakama Kuu, Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama ya Wilaya ni miezi sita, wakati Mahakama ya Mwanzo ni miezi mitatu, hali ambayo awali ilichukua takribani miaka minne.
Jaji Mfawidhi Katarina anasema, pamoja na kudhibiti vitendo hivyo, TEHAMA imeongeza kasi ya kusikiliza mashauri, uwazi na uwajibikaji.
Ametoa mfano kuwa, Mfumo wa Usimamizi wa Mashauri kwa Njia ya Kielektroniki (eCMS) umeimarishwa na kuunganishwa na taasisi 14 ambapo mteja anaweza kufungua shauri, kupata mwenendo wa shauri, hukumu, amri za mahakama, ratiba na malipo kwa njia ya mtandao.
Kwa mujibu wa Jaji Mfawidhi Katarina, taasisi hizo ni pamoja na Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), EWURA, RITA, NIDA, Magereza na Tume ya Usuluhishi na Uamuzi kwa Migogoro ya Kikazi.
Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe Balozi Dkt Batilda Burian, amerejea kauli mbiu ya maadhimisho hayo inayosema, “mchango wa Mahakama katika Ustawi wa Maendeleo ya Taifa”, na kusema mhimili huo unachangia kustawisha maendeleo kwa kutatua migogoro kwa wakati.
Amesema, hali hiyo inawafanya waadawa kwenye mashauri yao kupata haki kwa wakati, na kuendelea kutekeleza majukumu yao kiuchumi, kisiasa na kijamii.
Ametoa mfano kuwa, kumezuka migogoro mingi ya aridhi mkoani humo inayosababishwa na kupanda kwa thamani na wanachi kupata uelewe juu ya umuhimu wa rasilimali hiyo.
“Katika kudumisha amani, Mahakama imesikiliza na kuyatolea uamuzi mashauri hayo, na hatimaye wadaawa kuweza kupata haki zao na kuendelea na majukumu yao uzalishaji,” amesema.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Hamza Saidi Johari pamoja na mambo mengine, amesema kauli mbiu ya mwaka huu, inaakisi nafasi ya kipekee ya Mahakama katika kulinda haki, kudumisha amani na kuweka mazingira wezeshi ya kisheria, kimuundo na kitaasisi kwa maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
Kwenye hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Mwanasheria, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu Mkoa wa Tanga, Wakili Rebecca Msalangi, Johari amesema ustawi na maendeleo ya Taifa inahusisha uwezo wa wananchi kumudu mahitaji muhimu kama chakula, mavazi na malazi, ambapo kila muhimili, unapaswa kutimiza wajibu wake ipasavyo.
Naye Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Wakili Boniface Mwabukusi, maadhimisho hayo yanakumbusha kuwa, maendeleo ya Taifa yasingewezekana bila utawala wa sheria na Mahakama huru.
Hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Mwenyekiti wa TLS Mkoa wa Tanga, Mary Swai, imeeleza kuwa, Chama hicho kitaendelea kuwa mdau mwaminifu, mshauri wa kitaalamu kwa Serikali, Bunge na Mahakama, na mlinda maslahi ya haki na uwajibikaji katika Taifa.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.