Na Mashaka Mgeta, OMM TANGA
MKUU wa Mkoa wa Tanga, Mhe Balozi Dkt Batilda Burian, ameahidi kuratibu mpango wa kupata rasilimali zitakazoboresha huduma kwenye Mahakama Kuu Kanda ya Tanga, ikiwemo usikilizaji mashauri kwa njia ya mtandao.
Mhe Balozi Dkt Batilda ameyataja maeneo mengine ya uratibu ni upatikanaji wa ardhi kwa ajili ya ujenzi wa mahakama na ofisi zake, ili kuwafikishia wananchi huduma za kimahakama kwa karibu zaidi.
Ameyasema hayo leo Februari 2, 2026 kwenye Maadhimisho ya Siku ya Sheria, yenye kauli mbiu inayosema, “Mchango wa mahakama katika ustawi na maendeleo ya Taifa”, na kuongeza kuwa, uratibu huo ni mwendelezo wa ushirikiano usioathiri uhuru wa mihimili ya Bunge, Mahakama na Serikali.
Mhe Balozi Dkt Batilda amasema, kufanyika kwa maadhimisho hayo ni ishara ya wazi kwamba Tanzania inatambua na kuheshimu utawala wa sheria, kadri ulivyoakisiwa kwenye Katiba ya nchi.
Kwa upande mwingine, Mhe Balozi Dkt Batilda, amesema mahakama inachangia kustawisha maendeleo ya nchi kwa njia tofauti kama vile utatuzi wa migogoro ikiwemo ya ardhi.
Amesema, hali hiyo inawafanya wadaawa kupata haki kwa wakati, hivyo kutekeleza majukumu yao ya kiuchumi, kisiasa, kijamii na nchi kuendelea kunawiri katika nyanja zote.
Kwa mujibu wa Mhe Balozi Dkt Batilda, ongezeko la thamani ya ardhi na kukua kwa uelewa wa thamani ya rasilimali hiyo, ni miongoni mwa vichocheo vya migogoro ya ardhi mkoani humo.
Naye Mwanasheria Mkuu wa Mkuu wa Serikali, Hamza Saidi Johari amepongeza hatua zinazochukuliwa na Serikali baada ya vurugu za Oktoba 29, 2025.
Kupitia hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Mwanasheria wa Serikali Mkoa wa Tanga, Wakili Rebecca Msalangi, Johari amesema hatua hizo hususani kuundwa kwa Tume ya Uchunguzi, kutaweka msingi wa maridhiano ya kitaifa, kujenga na kudumisha umoja na mshikamano nchini.
Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Wakili Boniface Mwabukusi, amesema TLS iko tayari kushirikiana na Serikali na wadau wote kutafuta suluhu endelevu ya changamoto zinazohitaji nguvu ya pamoja kuleta ustawi wa maendeleo kitaifa.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.