Na Emma Kigombe
Serikali Mkoani Tanga imeendelea kuweka mazingira rafiki kwa wawekezaji hasa wa viwanda ili kuirudisha Tanga ya zamani ya viwanda na kuweka mazingira rafiki kwa wawekezaji wengine
Hayo yamebainishwa na Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe. Omary Mgumba katika ziara yake ya kutembelea viwanda mbalimbali mkoani humo ikiwa ni jitihada za kufuatilia utekelezaji wa maelekezo ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuirudisha Tanga kwenye hadhi yake ya viwanda.
Akizungumza mara baada ya kutembelea kiwanda cha kadi Mkuu wa Mkoa wa Tanga Omary Mgumba amesema kuwa Mkoa umeweka mazingira rafiki kwa wawekezaji wote ili kupata matokeo mazuri na kuwapa fursa wawekezaji kuwekeza zaidi.
" Tumeweka mazingira mazuri kwa ajili ya kuvutia wawekezaji na moja ya matokeo hayo ndio uwekezaji huu unaofanywa na kiwanda hiki cha pekee Afrika Mashariki ambapo kwa Afrika vipo viwanda viwili kimoja kipo Tanzania Mkoani Tanga na kingine Afrika kusini" alisema Mgumba
Aidha Mgumba ametoa pongezi kwa mwekezaji kwa kuichagua Tanga kufungua kiwanda hicho cha pekee ambacho kina manufaa makubwa kwa wananchi wa mkoa wa Tanga na Taifa kwa ujumla.
Pia Mgumba amesema ameridhishwa na maendeleo ya kiwanda cha uzalishaji kadi za kielektroniki ( smart card) kwa kuwa katika hatua za mwisho kuanza uzalishaji.
"Kama tulivyoshuhudia ,wapo katika hatua za mwisho ya majaribio za kutengeneza kadi za kimtandao kwa hiyo uwepo wa kiwanda hiki ni moja ya jitihada za Mhe. Rais Rais katika ujenzi wa viwanda na kutengeneza ajira kwa watanzania" aliongeza Mgumba
Sambamba na hilo Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mhe Omary Mgumba akatoa wito kwa wadau mbalimbali kuunga mkono jitihada za Mhe Rais katika kununua bidhaa zinazozalishwa kwenye viwanda hivyo.
"Nitoe wito kwa wadau wote ambao wanategemea kazi kwa ajili ya kazi zao kuja Tanga na kuonana na kiwanda hiki kuwapa tenda badala ya kupeleka nje ya nchi wazitengeneze kadi hizo hapa Tanzania kwa ajili ya kuokoa uchumi wetu na kutengeneza ajira nyingi kwa watanzania" alisema Mgumba
Kwa upande wake Mstahiki Meya wa Jiji la Tanga Abdurahman Shiloow amesema uwepo wa viwanda hivyo ndani ya Jiji na Mkoa wa Tanga vitasaidia kuwanufaisha wananchi katika suala zima la kupata ajira na kuiongezea serikali mapato kupitia kodi zinazolipwa na wawekezaji hao.
Nae mmiliki wa kiwanda cha kadi na vocha Rashid Liemba amesema kiwanda hicho kitakapo anza kufanya kazi kitatoa ajira kwa wananchi wa Tanga huku kikileta fedha nyingi za kigeni
" Biashara kubwa tunayoifanya tunapeleka fedha zetu nchi za nje kununua kadi lakini sasa hivi tunatengeneza kwenye nchi yetu mtusaidie katangaza soko lilipo" Alisema Liemba.
Katika hatua nyingine Mkuu wa mkoa Omary Mgumba ametembelea kiwanda cha vipodozi cha Ashers ambapo mara baada ya kupitishwa katika maeneo mbalimbali ya uzalishaji wa kiwanda hicho alisema kuwa amefurahishwa na kiwanda hicho kuwa ni miongoni mwa walipa kodi wazuri katika mkoa wa Tanga
"Kwa taarifa na takwimu nilizokuwa nazo kiwanda hiki kimekuwa kikilipa kodi vizuri na kwa wakati na kiasi ambacho tunakubaliana" alisema Mgumba
Aidha Mgumba alisema jambo kubwa alilovutiwa nalo katika ziara yake kiwandani hapo ambalo linatupa funzo sisi watanzania ni kuendeleza urithi ambao tumeachiwa na waazilishi wetu kwa kuwa kiwanda hicho mpaka sasa ni kizazi cha tatu na bado kinaendelea kufanya vizuri katika uzalishaji.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa kiwanda cha vipodozi Ashers Vanden Ashers ameishukuru serikali ya Mkoa wa Tanga kufika kiwandani hapo na kuchukua changamoto ambapo anaamini ujio huo utaenda kuleta mapinduzi makubwa kwenye sekta ya viwanda Mkoani humo.
Dhamira ya Serikali ni kuhakikisha Mkoa wa Tanga unarudi kwenye hadhi yake ya viwanda kwa kuwawekea mazingira rafiki wawekezaji wote mkoani humo.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.