MWENGE KUFUATILIA MILIONI 478 ZA KUMALIZIA MRADI WA MAJI HANDENI
Na Mashaka Mgeta, HANDENI
MWENGE wa Uhuru Kitaifa 2024, umeingilia kati na kuomba barua ya kukumbushia na kufuatilia Shilingi milioni 400 za kumalizia mradi wa maji Kwenkambala, uliopo wilaya ya Handeni mkoani Tanga.
Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2024, Godfrey Mnzava, amemuelekeza Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Mhe Albert Msando, kumpatia nakala ya barua ya kukumbushia malipo hayo, ili Mwenge wa Uhuru uwasiliane na Waziri wa Maji, Mhe Jumaa Aweso, kwa ajili ya kuongeza nguvu ya fedha hizo kutolewa zitumike kwa umaliziaji wake.
Mnzava, ametoa agizo hilo wakati Mwenge wa Uhuru 2024 ulipotembelea mradi wa Kwenkamba unaotekelezwa na Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira (HTM) kwa kutumia wataalam wa ndani (Force Account).
Mkurugenzi Mtendaji wa HTM, Mhandisi Yohana Mgaza amesema, utekelezaji wa mradi huo umefikia asilimia 70 na ili kukamilika kwake, zinahitajika Shilingi 478,693,408.20 kwa ajili ya ununuzi na ulazaji wa mabomba, ujenzi wa vituo, ujenzi wa chemba pamoja na gharama za usimamizi.
Amesema Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira (RUWASA) imeandika barua Wizara ya Maji kukumbushia kupewa kiasi hicho cha fedha, kauli iliyomfanya Mnzava, kuhitaji nakala ya barua hiyo kwa ufuatiliaji.
Mhandishi Mgaza amesema, lengo la mradi huo ni kutoa huduma ya majisafi na salama kwa wananchi wa kata ya Kwediyamba wapatao 5,746.
Amesema mradi huo ulioanza kutekelezwa Septemba 11, 20222, ulitegemewa kukamilka Septemba 10, 2023, lakini kutokana na fedha kutopatikana kwa wakati, haujakamilika hadi sasa na kwamba unatarajiwa kukamilika Juni 2024,.
Mhandisi Mgaza amesema mradi huo utagharimu Shilingi takribani bilioni 1.3 kutoka Serikali Kuu na kwamba hadi kufikia leo Aprili 19, 2024, HTM imepokea Shilingi milioni 800 kwa awamu tatu kuanzia mwaka 2022/23 na 2023/24.
Kwa mujibu wa Mhandisi Mgaza, zazi zilizopangwa kutekelezwa ni pamoja na ufungaji wa pampu ya kusukumia maji, kuchimba mtaro na kulaza bomba kuu la kipenyo cha milimita 110 (PN16 & PN10) umbali wa mita 5,925 na ujenzi wa tenki la kuhifadhia maji lenye uwezo wa kuhifadhi lita 150,000 kwenye Mnara wa mita 9 katika mtaa wa Mpakani.
Kazi nyingine ni kuchimba mtaro na kulaza mtandao wa mabomba ya kusambaza maji ya vipenyo kuanzia milimita 32 hadi 160 (PN 12.5 & PN10) kwa umbali wa mita 17,920, ujenzi wa vituo/vilula 29 vya kuchotea maji.
Aidha, Mhandisi Mgaza amesema wananchi wa eneo hilo wamechangia mradi kwa kutoa maeneo yao bure yenye ukubwa wa zaidi ya ½ ekari, yenye thamani ya Shilingi 5,000,000 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya mradi.
Amesema jumla ya Shilingi milioni 800 zimetumika kutekeleza shughuli za usanifu wa mradi na maandalizi ya michoro, ujenzi wa tenki lenye ujazo wa lita 150,000 kwenye mnara wa mita tisa, kuchimba mtaro na kulaza bomba kuu la kipenyo cha milimita 110 (PN16, PN 12.5 na PN10) umbali wa mita 5,925.
Shughuli nyingie ni kuchimba mtaro na kulaza bomba kuu la kusambazia maji kipenyo cha milimita 150 (PN 12 na PN10) umbali wa mita 2,000 na kuchimba mtaro na kulaza bomba la kusambaza maji lenye kipenyo cha milimita 63, milimita 50, na milimita 32 (PN10) umbali wa mita 1,650.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.