RC BATILDA AINGIA TANGA…ATAJA VIPAUMBELE 14
Na Mashaka Mgeta, TANGA
MKUU wa Mkoa wa Tanga, Balozi Dk Batilda Burian, ametaja vipaumbele 14 vitakavyomuongoza katika utumishi wake mkoani humo.
Mhe Dk Batilda amehamishiwa Tanga akitokea Tabora alipokuwa katika wadhifa huo, baada ya Mheshimiwa Rais Dk Samia Suluhu Hassan kufanya uteuzi na kuwabadilishia vituo vya kazi baadhi ya viongozi wa kuteuliwa Machi 9, 2024.
Mhe Dk Batilda amechukua nafasi hiyo kutoka kwa mtangulizi wake, Waziri Kindamba, aliyeteuliwa kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Mabasi Yaendayo Haraka (UDART).
Akizungumza katika hafla ya kumuapisha Mkuu wa Wilaya ya Mkinga, Mhe Evans Mtambi, Mhe Dk Batilda amevitaja vipaumbele hivyo kuwa ni kukuza kiwango cha elimu hasa katika ufaulu, uboreshaji wa huduma za afya na sekta ya kilimo na uvuvi.
Pia Mhe Dk Batilda amevitaja vipaumbele vingine ni miradi ya kimkakati na ubunifu wa fursa zinazotokana na miradi hiyo, ulinzi na usalama wa watu na mali zao, udhibiti wa mfumko wa bei hasa kipindi hiki cha mfungo wa Kwaresma na Ramadhani.
Mhe Dk Batilda amevitaja vipaumbele vingine kuwa ni kusikiliza na kutatua kero za wananchi, uimarishaji wa majukwaa ya uwezeshaji, utatuzi wa migogoro ya ardhi, usafi na hifadhi ya mazingira.
Vipaumbele vingine ni usimamizi wa maadili mema kwa jamii, lishe hasa kwa watoto wa chini ya miaka mitano na wanafunzi mashuleni, Mwenge wa Uhuru 2024 na uchaguzi wa serikali za mitaa, vijiji na vitongoji.
Amesema mafanikio katika kuleta ufanisi kwenye vipaumbele hivyo yanategemea zaidi ushirikiano na kutimiza wajibu kwa kila mtumishi wa umma mkoani humo.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Muheza, Mhe Zainab Abdallah amesema, uzoefu wa kitaaluma na kazi alizozifanya Mhe Dk Batilda vinatarajiwa kuwa nyenzo za kuchagiza kasi ya maendeleo na ustawi wa wananchi wa Tanga.
Mhe Zainab amesema wakuu wa wilaya, wakurugenzi watendaji wa halmashauri na watumishi wote wa umma kwenye wilaya nane za mkoani humo, wapo tayari kutoa ushirikiano, kupokea na kutekeleza maelekezo ya Mhe Dk Batilda, ili kufikia malengo ya utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Mwenyekiti wa Mkoa wa CCM, Ustaadhi Rajab Abdulrahaman amesema mabadiliko yanayofanywa na Mhe Dk Samia yamezidi kuineemesha Tanga kwa kuwa na viongozi wenye kutekeleza maono yake (Mhe Rais Dk Samia) katika kuwatumikia wananchi.
Ustaadhi Rajab amesema miongoni mwa maeneo ambayo CCM inatarajia kuona yakifanyiwa kazi kwa nguvu zaidi ni usafi na uhifadhi wa mazingira, hasa kwenye masoko ambapo hali ilibainika kuwa si ya kuridhisha.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.