Na Mashaka Mgeta, OMM TANGA
IKIWA imepita miezi miwili na siku 16 tangu aondoke mkoani Tanga Machi 1, 2025 alipofanya ziara ya kikazi, Mhe Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, anasafiri kwa reli iendayo kasi inayotumia umeme (SGR) kutoka Dar es Salaam kwenda jijini Dodoma, umbali wa kilomita 444.
Kupitia ukurasa wake wa Instagram, Mhe Rais Dkt Samia ameandika hivi:-“Treni yetu, Fahari yetu. Leo nimesafiri kwa treni ya SGR toka Dar es Salaam kwenda Dodoma. Hakika Watanzania tunayo kila sababu ya kujivunia hatua kubwa tunazoendelea kupiga kama Taifa”.
“Nikiwa Dodoma pamoja na kazi nyingine, nitaboresha taarifa zangu katika Daftari la Kudumu la Mpigakura katika Ofisi ya Kijiji, Chamwino. Ninawasihi wananchi wenzangu tuendelee kujitokeza kwa wingi kujiandikisha na kuboresha taarifa zetu, ili tutumie haki yetu ya kikatiba ya kushiriki Uchaguzi Mkuu, Oktoba mwaka huu.”
Hii si mara ya kwanza kwa Mhe Rais Dkt Samia kusafiri kwa treni hiyo, kwani Agosti 1, 2024, alifanya hivyo, ikiwa ni sehemu ya uzinduzi wa safari ya SGR kutokea Dar es Salaam Kwenda Dodoma. Pia, Novemba 23, 2024, Mhe Rais Dkt Samia alisafiri alitumia usafiri wa SGR kutoka Dar es Salaam hadi Stesheni ya Jakaya Kikwete mkoani Morogoro.
Wakazi wa Tanga wanaitathmini hatua hiyo ya Mhe Rais Dkt Samia kama sehemu ya viashiria vikubwa na chembechembe za uzalendo unaojikita katika kuthamini na kuzitumia rasilimali zinazotegemewa na wananchi wote.
Abdallah Chihumpu, mkazi wa Chanika mjini Handeni anasema, usafiri wa treni kwa jamii yetu unaonekana kuwa sahihi kwa watu wenye uwezo wa kati na hali ya chini kiuchumi, lakini si kwa viongozi hususani Mhe Rais.
“Mhe Rais Dkt Samia angeweza na anastahili kutumia usafiri wa ndege na magari yenye ulinzi mkali, lakini amekuwa akijishusha na kuungana na sisi raia wa kawaida kusafiri na treni, hii inazidi kumfanya anakuwa karibu sana na kwenye fikra za Watanzania walio wengi,” anasema.
Mkazi wa Lushoto, Herieth Sutta, anasema kitendo cha Mhe Rais Dkt Samia kutumia usafiri wa treni, pamoja na ubora wa miundombinu hiyo ya kisasa, lakini inaashiria salaam kwa Watanzania kuzipenda, kuzithamini na kuzitumia rasilimali zetu.
“Nchi imejaliwa rasilimali nyingi, imejaliwa viongozi bora kama alivyo Mhe Rais Dkt Samia, tuna miundombinu bora ya kisasa kama SGR na maendeleo makubwa katika sekta nyingine nyingi, hivyo nasi wananchi wa kawaida tunapaswa kuzithamini na kuwathamini viongozi wetu, kuzilinda na kuwalinda viongozi wengi,” amesema.
Mwenyekiti wa Jukwaa la Wenyeviti wa Vyama vya Siasa mkoani Tanga, Peter Mhina, anasema kitendo cha Mhe Rais Dkt Samia kutumia SGR kinatoa ‘picha’ ya ubora na usalama wa miradi iliyogharamiwa na Serikali, ikiwemo miundombinu ya reli hiyo.
“Kama SGR isingekuwa bora, imara na salama, siamini kama Mhe Rais angeshauriwa na kuutumia usafiri huo…tunajifunza kwamba miradi mingi kama si yote inayotekelezwa na Serikali yake, ni salama, imara na yenye ubora unaolingana na thamani ya fedha zilizotumika,” anasema.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.