Na Emma Kigombe, OMM TANGA
TAFITI zinaonesha kuwa kati ya asilimia 45 hadi 60 ya uharibifu wa ngozi inatokea wakati wa uchunaji ngozi kwenye machinjio, jambo linalochangia kwa kiasi kikubwa kushuka kwa ubora na thamani ya zao hilo muhimu kwa uchumi wa taifa.
Hayo yamebainishwa wakati wa ufunguzi wa mafunzo maalum kwa wakaguzi wa ngozi kutoka mikoa ya Tanga na Kilimanjaro, yaliyofanyika leo jijini Tanga kwa lengo la kuboresha mnyororo wa thamani wa zao hilo, kupitia usimamizi bora wa hatua zote za uzalishaji.
Akizungumza katika hafla hiyo, Kaimu Mkuu wa Idara ya Uchumi na Uzalishaji katika Sekretarieti ya Mkoa wa Tanga, George Mmbaga, amesema wachunaji ngozi ya wanyama wana mchango mkubwa katika kudhibiti ubora wa ngozi, hivyo ni muhimu kuwajengea uwezo kupitia mafunzo ya kitaalamu ya uchunaji bora.
Pamoja na mafunzo hayo, washiriki wamepewa vitendea kazi kama vile vitambulisho na nakala za sheria na kanuni za ngozi, ili kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi mkubwa.
Katika juhudi za kuinua tasnia ya ngozi nchini, Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ikiwemo uboreshaji wa koo za mifugo kupitia uhimilishaji na usambazaji wa madume bora, ukarabati wa majosho 762 na utoaji wa ruzuku ya dawa za kuogeshea mifugo.
Mikakati mingine ni pamoja na kutoa mafunzo kwa wachunaji 2,263, wapanga madaraja wa ngozi 75 na wakaguzi wa ngozi 113 na kugawa visu vya kisasa kwa ajili ya uchunaji bora.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.