Na Mashaka Mgeta, OMM TANGA
DHANA ya msemo wa ’mtembea bure si sawa na mkaa bure, huenda akaokota’ imedhihirika leo Mei 26, 2025 kwa baadhi ya wanawake wa kijiji cha Kilulu Duga, wilaya ya Mkinga mkoani Tanga.
Ingawa ’hawakutoka bure’ nyumbani kwao, walikwenda katika zahanati ya kijiji hicho kunapojengwa wodi ya mama mtoto, kushiriki ziara ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Mhe Balozi Dkt Batilda Burian, aliyefuatana na wajumbe wa Kamati ya Usalama (KU) kukagua mradi huo wenye thamani ya Shilingi milioni 35, utakaopitiwa na Mwenge wa Uhuru 2025.
Wanawake hao, Mwanaidi Mwaboga, Pili Makau, Fatuma Kikoya, Saumu Makau, Mwanaidi Hassan na Mariam Mzinga, wametakiwa kuunda kikundi na kubuni mradi wenye thamani ya kati ya Shilingi milioni 2 na milioni 3, kutoka kwa Mhe Balozi Dkt Batilda.
Pia, Mhe Balozi Dkt Batilda, ametoa majiko ya gesi kwa wanawake hao, kama ishara ya kuunga mkono mkakati wa matumizi ya nishati safi ya kupikia unaosimamiwa na Mhe Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, na kutekelezwa kwenye mataifa mbalimbali barani Afrika.
Mmoja wa wanawake hao, Pili Makau, amesema msaada wa fedha hizo utawainua kukuza uwezo wao wa uzalishaji bidhaa za kufuma, na kuyafikia masoko hasa yaliyopo jijini Tanga.
Naye Said Kibwana, mkazi wa kijiji hicho, alisema hatua hiyo ni yenye kuungwa mkono kwa viongozi wengine kuwa wasaidizi na wawezeshaji wa wananchi wanaohitaji kukua kiuchumi.
Kijana Mwikeni Omar, amesema ni miongoni mwa walionufaika na mkopo wa bodaboda kutoka kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga, hivyo kuwapa matumaini wanawake hao kuwa, fedha watakazopokea zitabadilisha maisha yao.
Mwenge wa Uhuru 2025 wenye kauli mbiu inayosema ”Jitokeze kwa wingi Kushiriki Uchaguzi Mkuu 2025 kwa amani na utulivu’, unatarajiwa kuwasili na kukimbizwa mkoani Tanga kuanzia Juni 6 hadi 17, mwaka huu.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.