Katibu Tawala Mkoa wa Tanga Pili Mnyema tarehe 3 Juni, 2024 amefanya ziara ya kutembelea na kukagua hatua ya mradi wa ujenzi wa Shule ya Sekondari ya wasichana ya Mkoa wa Tanga (Tanga girls) inayojengwa katika eneo la Mabalanga wilayani Kilindi.
Akizungumza mara baada ya kukagua ujenzi wa Shule hiyo Katibu Tawala amesema Serikali imetoa fedha kiasi cha shilingi Bilioni Tatu kwa ajili ya ujenzi wa Shule ya Mkoa ya wasichana lengo likiwa kuweka mazingira rafiki kwa watoto wa kike kupata Elimu bora na kuhamasisha kusoma masomo ya sayansi.
Mnyema amewataka viongozi wa Halmashauri ya wilaya ya Kilindi na mwananchi wa mabalanga kusimamia mradi huo kwa ushirikiano mkubwa ili kuhakikisha unakamilika kwa wakati na kufanya kazi iliyokusudiwa na Mhe Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kumpatia Elimu bora mtoto wa kike.
Mradi wa ujenzi wa Shule ya wasichana ya mkoa wa Tanga una jumla ya madarasa 12, mabweni nane, jengo la utawala, maabara tatu, nyumba za walimu , chumba cha wagonjwa, matundu ya vyoo ambapo vipo katika hatua ya umaliziaji pamoja na bwalo la chakula liliofikia asilimia 70.
Shule ya Sekondari ya wasichana ya Mkoa wa Tanga inatarajia kupokea kwa mara ya kwanza wanafunzi wa kidato cha Tano 122 kwa michepuo ya sayansi mapema mwezi Julai mwaka huu.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.