Serikali imesema wakati wowote kuanzia sasa kaya za wananchi wanaohamia kwa hiyari kutoka katika Hifadhi ya Taifa ya Ngorongoro kwenda Kijiji cha Msomera Wilaya ya Handeni, mkoani Tanga zitaanza kuwasili.
Hatua hiyo inatokana na kukamilika kwa nyumba 104 kati ya Zaidi ya 500 zinazoendelea kujengwa kwa ajili ya wananchi hao.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Pindi Chana amesema wakati akikagua miundombinu ya barabara, maji, mawasiliano, eneo la kuogeshea wanyama (josho), shule na zahanati ambazo ziko katika hatua za mwisho za kukamilika kwake.
“Nitumie nafasi hii kusema kuwa muda wowote kuanzia sasa kaya zitaanza kuingia tumejiridhisha huduma ya maji, shule, mawasiliano yako vizuri na tumeona kuwa iko haja ya kumalizia haraka barabara ili wafanye shghuli zao.
“Kama tunavyofahamu wananchi wale hawawezi kuendelea kukaa kule kwenye hifadhi kwa sababu kama mnavyofahamu kuna suala zima la wanayama, tumeona hali hii binadamu kukaa na wanyama haiwezekani leo hii mwaka 2022 unaweza kusema sawa lakini fikiria miaka 10 baadaye, watu wanaongezeka na wanyama wanaongezeka hali itakuwaje,” amesema.
Waziri Pindi amesema wananchi wana haki ya kupata elimu, kufanya biashara na mambo mengine lakini maeneo ya hifadhi haiwezekani kufanya shughuli zozote za maendeleo kama kumiliki ardhi kwa sababu kuna sheria zake hivyo eneo la kukidhi matakwa ya wananchi hao wanaotaka kuhamia kwa hiyari likatengwa Msomera.
“Maandalizi tunaona yanakwenda vizuri chini ya Mkuu wa Mkoa Tanga (Adam Malima) na timu yake na serikali iko makini kwanza kuwalinda wananchi wake tunasema kwamba haiwezekani wananchi na wanyama wakaishi pamoja katika eneo la hifadhi.
“Kwa hiyo nitoe rai sasa kwenu ndugu zetu wa Msomera watakapokuja hapa mpate kuwapokea wale ni ndugu zetu na tutaendelea kuwaonyesha maeneo, tuwapokee na tushirikiane nao ni ndugu zetu,” amesema.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Adam Malima amesisitiza uharakishwaji wa suala zima la mtandao wa mawasiliano ya simu za mkononi na miundombinu ya barabara ili kurahisisha huduma mbalimbali zikiwamo biashara na mahusiano.
“Ni vizuri hawa ndugu zetu watakapokuja basi mawasiliano ya simu za mkononi yawepo. Tunapotengeneza mji mpya kama hivi tunataka tuwe na uwezekano kwenye vyanzo mbalimbali vya kiuchumi kama mtu ana mifugo yake ana mnada Mombo basi aweze kupeleka mifugo yake huko yaani kitu kinachoifanya Msomera kuwa ya kuvutia ni ule uwezekano wa kwenda huku na huko bila bughudha tofauti na sasa ambapo safari ya dakika 45 unatumia zaidi ya saa moja na nusu,” amesema RC Malima.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Handeni, Sirieli Mchembe amesema wilaya yake iko tayari kuhakikisha wananchi wa Msomera na Ngorongoro wanaishi kwa amani na utulivu kama ndugu na tayari mipango bora ya matumizi ya ardhi yameandaliwa huku maeneo ya malisho, maeneo ya kukuza nyasi kwa ajili ya kipindi cha kiangazi ili mifugo isikose chakula yakitengwa.
Aidha, Mwenyekiti wa kijiji hicho Martin Parakech amesema kama tamko la Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa watu wataishi kwa Amani na hakuna atakayenyanyaswa ambapo pia ameiomba serikali kuwatengea shule ya kidato cha tano na sita.
Golf Area/Masiwani Road Tanga
Anuani ya posta: P.O.Box 5095 Tanga
Simu: 027 2642421
Simu ya Mkononi:
Barua pepe: ras.tanga@tamisemi.go.tz
Haki miliki ©2017 Katibu Tawala Mkoa wa Tanga . Haki zote zimehifadhiwa.